Friday, October 2, 2015

Kagoma Green estates kuongeza thamani ya zao la ndizi Kagera

Sasa ni dhairi kwamba juhudi za serikali katika kupambana na umasikini zinaanza kuzaa matunda baada ya watanzania wazalendo kuanza kuonyesha njia katika juhud za kuunga mkono juhudi hizo kwa kuwekeza katika sekta ya kilimo. Mtanzania mzalendo ambaye ameamua kuonyesha juhudi zake za kuondoa umasikini kuanzia kijijini alikozaliwa Ndugu Salum Said Seif kupitia kampuni yake iitwayo Kagoma Green Estates ameamua kuwekeza katika zao la ndizi ambalo anatarajia kuongeza thamani katika zao hilo kwa kuanzisha kiwanda cha juisi ya asili inayotokana na zao hilo. Akiwa mzaliwa wa kijiji cha Kagoma Salum mwenye kauli mbiu ya “Mjini ni Pori” anaamini kwamba huko ndiko watu wanakoenda kukata kuni wakimaliza wanarudi nyumbani kwa ajili ya kupikia, hivyo na yeye ameamua kurudi kuwekeza nyumbani ili watu wengine waige ili watanzania wengi waondokane na umasikini Kagoma Green estates ambayo imeamua kuweka shamba kubwa la mfano katika kijiji cha Kikuku Wilaya ya Muleba wamepanda ndizi za sukari kwa ajii ya kutengeneza juisi ya ndizi na kampuni pia inajihusisha na uhifadhi wa mazingira kwa kupanda miti katika sehemu mbalimbali na kulinda vyanzo vya maji Akizungumza na waandishi wa habari Meneja mradi wa Kagoma Green estates Bwana Sylivester Marosha Ihuya anasema mradi wao ni wa kipekeenchini Tanzania kutokana kwamba utanufaisha wananchi wote wa Kanda ya ziwa hasa wale wote wanaolima zao la ndizi. “Mradi wetu umelenga kuondoa umasikini na pia mkurugenzi wetu ambaye ni mzaliwa wa hapa anapenda kuona kile alichopata anagawana na wananchi wake. Tunataka tuisaidie jamii ya hapa, tutanunua mazao yao na kuwaletea maendeleo hapa walipo. Pia tumejitolea kujenga choo cha kisasa kwa ajili ya Ofisi ya serikali ya kata Kagoma ” anasema Marosha Marosha anasema kwamba ni mradi wa kusaidia zaidi jamii, kuondoa umasikini na pia kuiendeleza Kagoma na kanda ya ziwa kwa ujumla hasa kaya masikini ili wanufaike na mazao yao hasa zao la ndizi ambalo ndilo zao kuu la chakula na biashara katika kanda ya ziwa. “Tumeamua kulima ndizi ili tuiongezee thamani zao hili kibiashara kwa kuanzisha kiwanda cha kusindika juisi asili (organic juice) ambayo haitahitaji kuongezewa sukari kama matunda mengine” anasema Anasema kwamba soko lao litakuwa kwanza Kanda ya ziwa na badaaye juisi hiyo itasambazwa na maeneo mengine ya nchi ya Tanzania na ikiwezekana na nchi za nje. Tangu mradi wa Kagoma Green estates uanzishwe mapema mwaka huu, jamii ya wananchi wa maeneo ya jirani wamenufaika sana kwa kujipatia ajira ya kilimo, kuuza miche ya migomba, madereva wa kuendesha mitambo, wafanyakazi wa umwagiliaji, walinzi na pia jamii imenufaika kutokana na shamba lao kuwa shamba darasa. “Wananchi wa hapa wamenufaika sana na wataendelea kunufaika na kampuni yetu kutokana na shughuli zetu mbalimbali na pia shamba letu ni shamba darasa.Wataalamu mbalimbali wa kilimo wanafika hapa kwa ajili kutoa elimu inayohusu kilimo bora , matumizi bora ya ardhi na uhifadhi wa mazingira” anasema Marosha Kagoma Green estates pamoja na shughuli nyingine imejidhatiti katika utunzaji wa mazingira kwa kuvilinda vyanzo vya maji. Ulimaji wa shamba ni wakisasa kwa kutumia mbinu mbalimbali za kilimo cha kisasa “Unaona hapa tuko maili nyingi karibu mita 200 kutoka katika vyanzo vya maji na pia umwagliaji wetu katika shamba letu ni wa kisasa. Tunatumia mabomba kumwagilia na umwagiliaji wa drip (drip irrigation). Wafanyakazi wetu wanatumia vifaa bora vya kilimo na katika kupanda hatutumii mbolea za kemikali” anasema Naye msimamizi wa shamba Bwana Projestus Francis (32) anasema tangu azaliwe hajawahi kuona mradi kama huo unaletwa kijijini kwao huku akisema umekomboa vijana wengi wa kijijini hapo ambao walikuwa hawana shughuli maalumu. “Sina cha kusema ni mradi wa kihistoria ambao mimi na familia yangu hatutakuja kusahau. Mimi shughuli yangu hapa ni kuangalia kila kitu kinacholetwa hapa nakipokea mimi na kutoa risiti” anasema Projestus Anasema vijana wengi kijjini hapo na vijiji vya jirani wamepata ajira ya maana kwa sababu kila siku mwenye bidii anaondaka na shilingi 20,000/= kama ujirra wa kibarua. Hii ni pesa nzuri sana ukilinganisha walio wengi tulikuwa hatuipati hapo kabla “Malengo yangu kama mungu atasaidia yatatimia kwa sababu ninachopata hapa kinanisaidia sana mimi na familia yangu ambayo ina watoto watatu.Ninachoweza kusema ni kwamba vijana wachangamkie fursa hii haraka waje tuunde kikundi tufanye kazi kwa Kagoma Green estates kwa pamoja ili tunufaike na mradi huu” anasema. Pia kijana wa kisukuma ambaye amesafiri na wenzake kutoka Mwanza ambaye amekuja kuichangamkia fursa katika shamba la Kagoma Green estates Bwana Jonsina Makwaya anasema amefarijika sana kuona mradi huo unaletwa Kanda ya Ziwa. “Nimetoka Mwanza kuja kulima hapa na mazingira ni mazuri muno hapa na mradi huu ni wa kipekee kwa sababu pesa tunayolipwa hapa inakidhi mahitaji yetu hapa. Tumepewa nyumba tunaishi, tunakula na tunalipwa pesa nzuri nawashauri vijana waje wachangamkie fursa hii” anasema.